Test Footer

Home » » Halmashauri yagundua ubadhirifu dawa za mil.100/-

Halmashauri yagundua ubadhirifu dawa za mil.100/-

Written By mahamoud on Tuesday, May 15, 2012 | 12:39 PM

Halmashauri ya Wilaya ya Kilwa, mkoani Lindi imegundua udanganyifu na ubadhirifu mkubwa wa dawa unaofikia karibu Sh. milioni 100.
Mkurugenzi Mtendaji wa Halimashauri ya Kilwa Adoh Mapunda, alifichua kuwa udanganyifu huo unafanywa na baadhi ya watumishi wa halmashauri wanaopokea dawa hizo kutoka Bohari ya Dawa (MSD ) na kuziingiza katika zahanati hewa ambazo hata ujenzi wake haujakamilika.
Ripoti hizo zinakuja wiki chache baada ya Bunge kuchachamaa kutaka ubadhirifu wa fedha na mali za umma ukomeshwe kwenye halmashauri na serikali kuu, hatua iliyosababisha baadhi ya Mawaziri kuwajibishwa wakiwemo Waziri wa Afya na Ustawi wa Jamii,
Mapunda , alikifahamisha kikao cha Baraza la Madiwani kilichofanyika hivi karibuni juu ya ubadhirifu huo na kuongeza kuwa kwa miaka mitatu watumishi hao wameiba madawa yenye thamani ya Sh. milioni 83.2 kwa kuyaingiza kwenye zahanati hewa.
Alisema kiasi hicho cha dawa zilihujumiwa katika kipindi cha mwaka 2007 hadi 2010 kwa kusingizia kuwa kinapelekwa katika zahanati nane ambazo ujenzi wake haujakamilika.
Alizitaja zahanati hewa mbele ya baraza hilo kuwa ni Mitole, Hoteli Tatu, Kiranjeranje, Kisongo, Mchakama, Nangurukuru pamoja na vituo vya Mikole na Kimbalambala.
Kwa mujibu wa taarifa ya mkaguzi wa hesabu wa ndani iliyosomwa na mkurugenzi huyo alibainisha kuwa ukaguzi umeibua kuwepo vituo vinane ambavyo ujenzi wake haujakamilika lakini vimepatiwa usajili na kila kimoja hutengewa gawio la Sh milioni 7.3 kwa ajili ya dawa. Mkaguzi wa ndani alifanya uchunguzi wake katika vituo 51 vya kutolea huduma za matibabu.
Mkurugenzi huyo alieleza kuwa katika ukaguzi wa ndani ambaye yeye mwenyewe alimpatia jukumu la kufuatilia hujuma hizo mara baada ya kuhamishiwa kwenye halmashauri hiyo, imegundulika kuwa, vituo viwili kati ya hivyo vinane vilipewa gawio la dawa za thamani ya Sh.milioni 14.7 kila kimoja na vilivyosalia vilipata gawio la dawa za thamani ya Sh. milioni 7.3 kila kimoja.
Kutokana na takwimu zilizotolewa na Mkurugenzi wa Halmashauri inaonyesha kwamba madawa ambayo yalipelekwa kwenye zahanati hizo nane hewa yana thamani ya Sh. milioni 83.2 na haijafahamika mgao huo wa madawa ulikuwa ukipelekwa wapi.
Mapunda aliliambia baraza hilo la madiwani kuwa hali hiyo ni hujuma kubwa kwa serikali ambapo imeisababishia halmashauri kukumbwa na tatizo la kupelekewa dawa zisizohitajika, kwa maana kwamba kiasi hicho cha madawa kingeweza kupelekwa katika sehemu nyingine nchini.
Halmashauri ya wilaya ya Kilwa ina jumla ya zahanati 43, Vituo vya Afya vitano na hospitali mbili.
Baraza la madiwani ambalo lilimpongeza mkurugenzi huyo kwa kufanikisha kugundua ufisadi huo na lilipitisha azimio la kuwafikisha kwenye vyombo vya sheria, watumishi wote wanaotuhumiwa kufanya udanganyifu wa kupokea dawa kutoka Bohari ya Dawa na kuziingiza katika zahanati hewa.
Akizungumza kwa niaba ya madiwani wenzake, Mahadhi Nangoma, Diwani wa Lihimalyao, alisema hoja hizo zinapaswa kufanyiwa kazi ipasavyo ili iwe fundisho kwa watendaji wenye tabia ya kutumia vibaya madaraka yao.
Vitendo hivyo vya ubadhirifu vilifanyika wakati ambapo wakurugenzi zaidi ya wanne walikuwa wamefanyakazi katika Halmashauri ya Wilaya ya Kilwa kabla ya Mkurugenzi wa sasa kuhamishiwa katika halmashauri hiyo na kugundua ubadhirifu huo.
SOURCE: NIPASHE JUMAPILI
Share this article :

0 comments:

Post a Comment

 
Support : Creating Website | Johny Template | Mas Template
Copyright © 2011. KILWA FORUMS - All Rights Reserved
Template Created by Creating Website
Proudly powered by Blogger